Saturday, July 22, 2017

CCM yambana Mkurugenzi Singida

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Manispaa ya Singida kimembana Mkurugenzi wa manispaa hiyo na kumtaka aweke sawa mambo kadhaa, ikiwemo kukipatia nishati ya jua kisima cha maji kilichopo kijiji cha Mtamaa ili kupunguza gharama za uendeshaji.
Masuala mengine ni pamoja na kujenga upya kibanda cha wauza tumbaku kwenye Soko Kuu na kuhakikisha magari yote madogo ya abiria yanayoegeshwa kwenye kituo rasmi kilichopo eneo la Misuna, viwanja vya UVCCM.
Chama hicho kimedai kuwa hatua ya kuweka nishati ya jua kwenye kisima cha Mtamaa itawezesha kupunguza bei ya ndoo moja ya maji kutoka Sh 50 hadi Sh 20, gharama ambayo inadaiwa wananchi wengi wa kawaida wataweza kulipa bila shida.
Katibu wa CCM Manispaa ya Singida, Sylvester Yaredi alitoa maagizo hayo juzi wakati wa ziara yake ya kikazi kukagua utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa chama hicho tawala.
Kauli ya katibu huyo imekuja baada ya baadhi ya wananchi wa kijiji cha Mtamaa kulalamikia bei kubwa ya ndoo moja ya maji kuuzwa Sh 50, wakidai ni kubwa kwa wananchi wa kawaida kuweza kumudu hali inayosababisha wakimbilie maji yasiyo safi na salama kwenye madimbwi.

No comments:

Post a Comment